London, Uingereza – Mei 2025:
Mamlaka ya Ushindani na Masoko ya Uingereza (CMA) imetoa ripoti yenye athari kubwa kwa sekta ya teknolojia, ikihitimisha kuwa makampuni mawili makubwa — Apple na Google — yamekuwa kikwazo kwa uvumbuzi na ushindani katika soko la vivinjari vya rununu (mobile browsers).
Katika ripoti hiyo ya mwisho iliyotolewa Jumatano, CMA inalaumu sera za Apple zinazowalazimisha watengenezaji wa vivinjari vya iOS kutumia injini ya kivinjari cha WebKit, hali inayopendelea kivinjari cha Safari na kudhoofisha uwezo wa ushindani wa vivinjari vingine. Vilevile, imeangazia mapungufu katika uwezo wa programu nyingine kuvinjari kwa uhuru pamoja na Safari kuwekwa kama chaguo-msingi kwenye iPhones.
Kwa upande wa Google, uchunguzi umebaini kuwa kivinjari cha Chrome kimewekwa kama default kwenye vifaa vingi vya Android. Zaidi ya hapo, Google inalipa kiasi kikubwa cha mapato ya utafutaji kwa Apple ili kuendelea kuwa injini ya utafutaji chaguo-msingi kwenye iPhones, jambo ambalo linapunguza motisha ya mashindano baina yao.
“Ushindani kati ya vivinjari vya rununu haufanyi kazi kama inavyotakiwa, na hali hii inakwamisha uvumbuzi nchini Uingereza,” alisema Margot Daly, mwenyekiti wa kikundi maalum cha CMA.
Athari kwa Watumiaji na Sekta ya Kidijitali
Ripoti inasisitiza kuwa kwa pamoja, Apple na Google wanatawala soko la vivinjari kwa kiasi kikubwa — Safari pekee inakadiriwa kushikilia asilimia 88 ya matumizi ya vivinjari kwenye vifaa vya Apple. Hali hii inafanya kuwa vigumu kwa watoa huduma wapya kuvutia watumiaji au kuleta teknolojia mbadala.
Majibu ya Apple na Google
Apple imejibu kwa tahadhari, ikisema:
“Tunaamini katika mazingira ya ushindani na uvumbuzi. Tuna wasiwasi kuwa mapendekezo haya yanaweza kuhatarisha faragha, usalama, na matumizi bora kwa wateja wetu.”
Kwa sasa, CMA haijachukua hatua za moja kwa moja. Badala yake, imezindua uchunguzi tofauti kwa kampuni zote mbili ili kubaini iwapo zinatawala soko la kidijitali kwa namna ya “kifedha na kimkakati.” Ikiwa zitapatikana na hatia, Apple na Google zinaweza kuwekewa masharti magumu ya kisheria au kutozwa faini inayoweza kufikia hadi asilimia 10 ya mapato ya kila mwaka.
Uchunguzi huo unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwaka huu.